Tuesday, March 18, 2014


KIMENUKA! Hospitali ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam imebainika kuwa na uzembe uliopitiliza, hali inayowafanya wagonjwa kuendelea kuilalamikia kila kukicha, Uwazi lina mlolongo wote.
OFM wakiwa na mgonjwa wao mapokezi hospitali ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam wakakuta patupu.
Uzembe huo umebainika baada ya makachero wa Oparesheni Fichua Maovu ‘OFM’ kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi wanaopata huduma duni katika hospitali hiyo huku wakilalamikia uzembe wa matabibu na rushwa kwa baadhi ya wahudumu.
Mtoa habari wetu alieleza kinagaubaga akidai kuwa mambo hayo husababisha wagonjwa kupoteza maisha kwa sababu ya kutopata huduma kwa wakati unaostahili au kwa kukosa fedha ya kutoa rushwa.
OFM wakimpeleka mgonjwa wao mapokezi hospitali ya Mwananyamala.
“Jamani OFM tusaidieni, hapa Hospitali ya Mwananyamala kuna matatizo sana. Unaweza kuja na mgonjwa wako lakini akakaa mapokezi hata nusu saa kabla ya kupata matibabu, halafu baadhi ya wahudumu wanapokea sana ‘kitu kidogo’.
“Hali hii inasababisha wagonjwa kufariki dunia na ndiyo maana mara nyingi utasikia mgonjwa alikufa kwa sababu ya kuchelewa kuhudumiwa kwa uzembe wa wauguzi,” alisema mwananchi huyo.
...OFM wakitafuta Machela eneo la hospitali ya Mwananyamala.
OFM MZIGONI
Baada ya kunasa maelezo ya mtoa habari wetu, OFM inayoendeshwa na Global Publishers ilifanya uchunguzi wa awali ambao ulibaini kuna ukweli kwenye madai hayo.
OFM YATUA MWANANYAMALA
OFM ikiwa imejipanga sawasawa, ilitinga hospitalini hapo Machi 13, mwaka huu saa nne asubuhi.
Nje ya hospitali hiyo ambapo OFM waliegesha gari, paparazi wa kike alijifanya mgonjwa sana na kubebwa na wenzake wawili waliojifanya mume na shemeji mtu.
...OFM wakichukua machela.
Ilikuwa saa 4:31 asubuhi ambapo makachero hao wa OFM wakiwa na ‘mgonjwa’ wao juu kwa juu, walipishana na madaktari waliokuwa wakizungumza bila kumjali mgonjwa huyo aliyebebwa huku  ‘akilalamika’ kwa maumivu makali.
MAPOKEZI SIFURI   
Katika eneo la mapokezi ya hospitali hiyo, makachero wetu hawakukuta mhudumu yeyote na kwa zaidi ya dakika 15 hakuna aliyetokea.
Waliendelea kubaki hapo wakiwa na mgonjwa wao aliyekuwa akiendelea ‘kulalamika’ kwa maumivu.
OFM (kushoto) wawapita madaktari wakiwa bize na mazungumzo yao.
OFM WAJIHUDUMIA
Ilibidi OFM hao wajihudumie wenyewe ambapo mmoja wao alifuata kitanda cha machela umbali wa mita kama ishirini na alipofika mapokezi, alitokea mtu mmoja aliyejitaja kuwa ni daktari na kuwataka OFM kumpeleka ‘mgonjwa wao’ katika chumba cha huduma ya kwanza.
NDANI YA CHUMBA CHA KITABIBU
Ndani ya chumba cha wagonjwa, OFM walikuta madaktari wa kike wawili (majina kapuni) ambao walimwelekeza mkuu wa msafara wa makachero kwamba anatakiwa akachukue kadi ya mgonjwa mapokezi kwenye dirisha la malipo.
MALIPO TATA
Awali kachero wa OFM aliambiwa alipie shilingi 6,000 na kipimo shilingi 2,000 lakini alipopeleka kadi ndani ya chumba cha wagonjwa, nesi mmoja (jina kapuni) alimwomba shilingi 8,000 bila ya risiti.
MGONJWA’ APIMWA, AKUTWA NA PRESHA
‘Mgonjwa’ wa OFM alipimwa na kubainika alikuwa na presha ya kushuka. Awali manesi walitaka kuelewa chanzo cha ugonjwa wa mgonjwa huyo ambapo walielezwa kuwa anasumbuliwa na mapepo.
OFM wakiwa mapokezi na mgojwa wao. Kuchsoto ni daktari aliyekuwa akitoa maelekezo tu bila kutoa msaada wowote
ALIMWA DRIPU MBILI
Baada ya kuibaini presha hiyo, madaktari walimtundikia dripu mbili za maji mgonjwa huyo ambazo hazikutolewa ufafanuzi wake licha ya kuzimaliza zote.
MGONJWA AAGWA
Baada ya kumaliza dripu hizo ambapo ya mwisho iliisha saa 5:57, mgonjwa huyo aliagwa na manesi huku wakitoa ushauri kwamba kwa vile alipata tatizo la presha ya kushuka wakijumlisha na mapepo, alitakiwa kunywa maji mengi na kufanya jitihada za kumpeleka kwa Askofu Kakobe kwa maombezi.
“Mpelekeni kwa Kakobe akaombewe, mjitahidi kumpa maji mengi ili kupunguza tatizo lake kama tulivyowafafanulia awali,” alisema nesi mmoja.

VIONGOZI WABANWA, WAJITETEA
Baadaye, OFM wengine wawili ambao hawakuwa kwenye zoezi la kwanza, walitua Mwananyamala kuonana na Meneja wa Kitengo cha Wagonjwa wa Nje (Outpatient Manager) aliyejitambulisha kwa jina la Meckrista Mashauri.
Alisomewa mashitaka huku akioneshwa picha za matukio ya asubuhi ambapo naye  alijitetea kwa kusema:
“Kweli kuna ukosefu wa huduma bora hasa maeneo ya mapokezi ambapo kutokana na uhaba wa wafanyakazi, kwa siku hupangwa mmoja tu.
“Mtu huyo huwa na kazi ya kuwapokea wagonjwa na kuwapeleka wodini, pia ikitokea dharura mtu huyo wa mapokezi hupaswa kumpeleka mgonjwa katika hospitali nyingine kama vile Muhimbili, hivyo kwa vipindi hivyo sehemu hiyo hukosa kabisa mtu wa kusimamia.
Akijibu tuhuma za kuwepo kwa rushwa katika hospitali hiyo, mkuu huyo alisema kuwa wao kama viongozi wamejitahidi sana kukomesha vitendo hivyo kwa matangazo na hata kuwepo kwa huduma za kielektroniki (Max Malipo) kwa kila malipo yanayofanyika hospitalini hapo:
“Hivyo kama kuna rushwa itakuwa inaendelea hiyo ni kutokana maslahi ya mtoaji na mpokeaji mwenyewe.
“Nawataka watu wanaokuja kupata huduma hapa hospitalini watambue kwamba wahudumu hapa wanafanya kazi sana tofauti na watu wanavyotuchukulia.
“Unakuta mhudumu mmoja anayetakiwa kisheria kwa siku kuwahudumia wagonjwa wanne, anawahudumia zaidi ya wagonjwa 40 kwa siku. Hii ni kutokana na wafanyakazi kuwa wachache, tunaomba watu watambue hivyo,” alihitimisha.

0 comments:

Post a Comment